Hivi ni kipi hasa ambacho wameweza kutueleza hadi sasa ambacho kweli kinahalalisha uwepo wao katika kinyang’anyiro hiki, achilia mbali kuchaguliwa kutuongoza? Ndio, ni kipi hicho ambacho nyie mmekiona mnisaidie maana mimi sijasikia chochote cha maana zaidi ya makelele yale yale tuloyazoea toka enzi na enzi.

Sana sana jipya ambalo mimi nimeliona hapa ni mbinu mpya za kupakana matope na kuchezeana rafu au wengine wanaziita faulu, kufanyiana fujo, kudhibitiana, kutunishiana misuli na vifua na mambo mengine kama hayo?

Ni nani hasa ambaye anaweza kunipa ushahidi wa dhati ambao hata nafsi yake inakiri kuwa ni wa kweli, kuwa hakuna mambo kama hayo katika hii tamthilia ya ‘Kuelekea IKulu ya Tanzania 2005′? Hakika kama yupo anaweza kunisaidia nami kujua maana Duniani ni kuelimishana.

Wakati naambiwa kuna wanaotishia kuwa watalala barabarani, wapo ambao walisema mkilala sisi tutahamia kwenye nyumba zenu, wakati kuna sehemu ni wazi kuwa kuna wagombea wanakataliwa, naambiwa pia kuwa bado jamaa wanaendeleza sera ya kuhimiza mafiga matatu, lakini limeibuka kali zaidi hivi karibuni. Eti matumizi ya bendera ya taifa katika kampeni ni uzushi sijui au makosa kama wenyewe walivyosema.

Hivi ni uongozi wa wapi ambao nyie mnawania au kugombea kama sio wa Tanzania? (Labda mhishimiwa Mchunga kondoo aliyegeukia Si-Hasa za Bongo, maana yeye anawania U-Rahisi wa Danganyika), pengine yeye ndiye hakutakiwa au ndio maana hajishughulishi nayo ati!!), na kama ni hivyo mnataka mbebe au hao wengine wabebe bendera za taifa gani? Ni utaifa upi ambao unapigiwa kelele huko majukwaani kama hata kutumia tu bendera ya taifa ni uzushi?

na ni hapa ninapojiuliza kuwa hiki wanachokinadi hawa jamaa zetu ni Demokrasia au ni Midomo ya Ghasia??