MWENYEKITI wa Chama ca Demokrasia na Maendeleo (CHADEMA), Bw. Freeman Mbowe hihi karibuni wakati anakubali uteuzi uliofanywa na chama chake kuwa awe mgombea wa nafasi ya Urais kwa tiketi ya chama hicho, alitoa risala moja ambayo ilikuwa tamu sana kuisikiliza. Tamu kwasababu kama kawaida, alijitahidi kuonyesha kiasi gani Wanasiasa wetu wanaendelea kufanya vyema katika Usanii wa kuunda maneno ili kuzidi kuwashika Wadanganyika. Katika risala hiyo kuna sehemu alisema eti :”Tanzania imemwagiwa Mafuta ya Taa na kwamba anahitajika kichaa mmoja tu ajitokeze ili kuwasha njiti na kisha italipuka (tehe tehe tehe!!!)

Inashangaza sana hakika kusikia hayo, hasa kwa mtu ambaye alinitangulia mimi kwa miaka kibao kuwasili duniani, kwasababu ukimuuliza mtu kama huyu kuwa huko awali walikuwa wapi wakati nchi inamwagiwa mafuta ya taa, utaanza kusikia longo longo za kumwaga ati. Nashindwa kuwaelewa hakika hawa jamaa zangu wanasiasa wanaposema kuwa eti hali imekuwa mbaya wakati wengi wao kama sio wote walikuwemo katika mchakato wa kuifanya hali hiyo mbaya wakati huo!

Mimi nadhani Bw. Mbowe alitakiwa kueleza ukweli kuwa Wanasiasa wetu kwa ujumla wao, walishiriki katika kuimwagia Tanzania mafuta hayo ya taa enzi hizo na sasa wanachojitahidi kufanya ni kukausha mafuta hayo japo kazi hiyo inawashinda.